Subject Index 
Search
Announcements
Feedback
Husseini Mwana wa Ali

Naanziliza kwajina

Lake yeye Subhana

Mola asiye kijana

Wala mke asiliye

   

Ndie watangu natangu

Kabula ya ulimwengu

Muumba nchi na mbingu

Milele Atabakiya

   

Asie na mshirika

Na wala hakuzalika

Ameketi pasi shaka

Enzie imetimiya

   

Sasa penda kuweleza

Kisa kenye kuchukiza

Na moyo nitaukaza

Hadi mwisho kufikiya

   

Ni rafiki wa Rasuli

Muhammadi mur sali

Husseini mwana wa Ali

Na Fatuma Hashimiya

   

Kipenzi chake Nabiya

Kuliko viumbe piya

Uhai wake sikia

Husseini akimwambiya

   

Wewe mtu wa peponi

Huna shaka asilani

Apendae kubaini

Namtizame Husseini

   

Baada kufa Rasuli

Muda ulipotawili

Na Alii mjamali

Mipoaga duniya

   

Kukazidi wasiwasi

Ulimwengu ukahisi

Pasiwe mwenye nafasi

Matumbo kupiganiya

   

Baada yote kufika

Na damu zikimwaika

Waso haya wakatoka

Vita wakaandaliya

   

Vikaandaliwa vita

Na mengi mno matata

Umbea nausalata

Vigaro vikatimiya

   

Vigaro vya mahasidi

Nyoyo zenye ufisadi

Chini ya yeye yazidi

Vitani wakaingia

   

Husseini yuko ndiani

Kutaka ihami dini

Kuwapinga mashetani

Nakuituza duniya

   

Kwa moyo uso imani

Majeshi yakawa kani

Na damu waitamani

YaHusseni na dhuriya

   

Wakawa wajikatakata

Watakayo washapata

Naimamu washamwita

Mjini kwao kungiya

   

Habari hiyo hanayo

Amekaza wake moyo

Kumbe mambo sasa siyo

Mauti yamngojea

   

Yunjiani enda zake

Akaweta watu wake

Waume na wanawake

Na radhi akawiliya

   

Kuwajuza kwa yakini

Hila zote kwa makini

Pasipo matumaini

Iraqi kufikiliya

   

Kawambiya kimbieni

Atakae samahani

Ela mini niwacheni

Nimuhali kukimbiya

   

Baada yeye kukuli

Wengi hawakuhimili

Kama vile mafahali

Nyumbani wakarudia

   

Akabakiya Husseini

Na dhuriya wa nyumbani

Na baadhi ikhiwani

Akali wakasaliya

   

Alipofika Iraqi

Jamii ya halaiki

Furaha na kujinaki

Jeshi likamwingilia

   

Akawa hana namna

Pande zote amebanwa

Pamwe na wake vijana

Wapi watakimbiliya

   

Akasema kwa lafudhi

Ka fasaha na mahadhi

Adui kuwapa radhi

Kuwatajia Jalia

   

Akawaonya mifano

Hati zao za mkono

Barua zilizo nono

Walizo kumwandikia

   

Kayesha yote maneno

Wala pasipo usono

Yote yasiwe ni neno

Yao wakashikilia

   

Wakamuonya adhabu

Na nyingi mno sulubu

Zimewaingia ghadhabu

Bila sababu ya njia

   

Adui pasi kuchoka

Wakamwandama M-maka

Karbala wakafika

Kusudi wa mwandamiya

   

Furati wakaushika

Pasi nafasi kutoka

Mto wakauzunguka

Na maji wakijinyweya

   

Kiu ikazidi sana

Najoto likawabana

Imamu na wake wana

Dhiki ikawadhidiya

   

Ikawa hakuna budi

Dhiki imeshawazidi

Wazee kwa auladi

Roho zikiteketea

   

Kiu ilo kubwa mno

Joto lisilo kifani

Vijana wazi midomo

Maji wanahitajiya

   

Maji wanywayo wanyua

Punda farasi na kima

Mjukuu wa Hashima

Adui akawendeya

   

Akenda kwao salama

Karibu roho kutema

Abdallah anawana

Kwa kiu kumzidiya

   

Kile kijana swaghiri

Imamu wetu Amiri

Tamaa hakukasiri

Ya mali kumpatiya

   

Adui wasikubali

Japo lau tone mbili

Mahali wakaratili

Pasi imani kuingiya

   

Mipo akikariri

Imamu akihubiri

Alipata takisiri

Chembe wakamrushiya

   

Wakamba ha ndiyo maji

Katu huyaonji maji

Mnyweshe yamfereji

Ni leo mtatubiya

   

Kijana kikalalama

Chembe limeshika nyama

Na damu mwili nzima

Mikononi kikafiya

   

Mikononi mwa Imamu

Yote ikajaa damu

Na roho yake ghulamu

Ikaiaga duniya

   

Katu wakamba adui

Maji yetu situmai

Mtayaona jamii

Kanwani hamtotiya

   

Ukazidi ukaidi

Kwa jeshi la mafisadi

Ikawa hapana budi

Roho zikiteketeya

   

Basi huu ndiyo mwanzo

Wakazidisha mikazo

Pasiwe hata pumbazo

Vitoto vikiumiya

   

Kajaribu kwa upole

Kuwaeleza walo pale

Maji yote yako tele

Japo tone kutumiya

   

Akenda huko karibu

Kiu ilimughilibu

Alipotaka jaribu

Chembe kikamuingiya

   

Kikamwingia Imamu

Chembe chao mahasimu

Mdomoni kikadumu

Na damu ikamweneya

   

Huku kiu imemshika

Damu ikichirizika

Msiba umemfika

Hana pakukimbiliya

   

Kakishika kakizuwa

Kwa nguvu akakitowa

Kamshukuru Moliwa

Muumba wa waja piya

   

Zikazidishwa sulubu

Mno na nyingi taabu

Rafikize wakaghibi

Mauti kuyandamiya

   

Rafiki wakaanguka

Imamu kumzunguka

Na damu zikimwaika

Akawa aogeleya

   

Katikati kwenye damu

Adui wakakalimu

Katu yako hayatimu

Mauti yakungojea

   

Mauti yenye taabu

Usumbufu na adhabu

Yatakufika karibu

Kaa ukiliadhania

   

Ni leo, leo ni leo

Utaiona kwa leo

Na wote hao watu

Wote tutawalemeya

   

Kakalimu muungwana

Kamshukuru Rabana

Na Molawe kalingana

Na dua kujiombeya

   

Akatamka Husseini

Kamwambia Mola manani

Kwako wewe shukrani

Nyoyo zimefurahiya

   

Hatuna katu huzuni

Kwa ulio yasaini

Mauti twayatamani

Kuliko kuangukia

   

Vita vikauma sana

Pasipo kusemeyana

Na Imamu akawana

Pasi nyuma kurejeya

   

Lakini ifae nini

Kwa adui elfeni

Na ziyada ilondani

Husseini akalegeya

   

Akalegeya kwa dhiki

Aloikuta hilaki

Asimpate rafiki

Huruma kumuonea

   

Ukweli ulodhihiri

Ikakabili ni shari

Haikuweko ni siri

Shida zikawachachiya

   

Kutamka kwa upole

Pasipo nyingi kelele

Sahibuze kuwambile

Atakaye kukiribiya

   

Usiku huo gizani

Kawambia kimbiyani

Namimi radhi moyoni

Na dua nawaombea

   

Jamii wakakataa

Heri kwao kujifia

Kuliko kuyakimbia

Mauti wakaridhiya

   

Adui likadhihiri

Moyo umetahayari

Na upesi ikaswiri

Imamu kumjiliya

   

Mtoto wake Husseini

Naye alipobaini

Karuka pasi makini

Amie kumteteya

   

Pasi khofu wala shaka

Adui akamshika

Na maneno katamka

Msihaya kamwambiya

   

Kamwambiya huna haya

Bure wayatenda haya

Utaikuta hizaya

Mbele ya Mola jaliya

   

Adui likazunguka

Mtoto akamshika

Husseini akimtaka

Kijana kumuusiya

   

Huku mepiga pambaja

Na adui huko waja

Na huku akiwapiga

Mpaka mwisho kufikiya

   

Yakamzidi machungu

Akamsabihi Mungu

Akaaga Ulimwengu

Mjukuu wa Nabiya

   

Ghafula akijiliwa

Roho yake ikatwawa

Adui lake Moliwa

Imamu akamwendeya

   

Akamwendeya kwa dhati

Akamendesha mauti

Jiadui afiriti

Dharuba kumwemezeya

   

Alipokufa Husseini

Yalitimu thelathini

Na tatu yaliyo ndani

Mafumu yalowingiya

   

Kuna tena thethini

Na nne mwake mwilini

Panga za hao wahuni

Mwilini zimesaliya

   

Mbali mengi majaraha

Kuyataja ni karaha

Moyo hauna furaha

Kwa Imamu kujifiya

   

Ndio huo mwisho wake

Hiki ndicho kisa chake

Cha Imamu tusichoke

Milele kujisomeya

   

Walipokwisha saini

Adui wakabaini

Sasa hii ni yakini

Ushindi umewajiya

   

Wakendewa majohari

Mabanati wa Amiri

Matekani wakaswiri

Huku wakiwachezeya

   

Pasi haya za uso

Wakaona ni kifani

Kuwatia taabani

Jamaa zake Nabiya

   

Wakazidisha jeuri

Wala pasipo na siri

Na kichwa chake Amiri

Fumoni wakakitiya

   

Huku wakikichezeya

Na huku wakiimbiya

Pasi imani kuwaingia

Wote wamefurahiya

   

Njiani walikipita

Nyoyo zao mezipata

Zimekwisha jaa vita

Shetwani amewaingia

   

Alipopata habari

Kwa ambayo yamejiri

Yazidi akaamuri

Ili kwehwa kumwiliya

   

Furahani vibaraka

Haraka kukipeleka

Kwa Yazidi kikafika

Meyowe kufurahiya

   

Akawa kukitozeya

Na vijiti kukitiya

Huku akimbiliya

Chini kukiumbiriya

   

Msihaya wake dini

Yazidi akatamani

Uchunguwe wa moyoni

Utatowa kwa duniya

   

Na huku akikigota

Meno akiyaambata

Uovu na usalata

Hakuna alodhaniya

   

Ajabu hii ajabu

Kwa kijanache swahibu

Kumfikiya ikabu

Wala pasipo hatiya

   

Muili ukiwa mbali

Kijana cha Murisali

Wakawachiwa mahuli

Na nyama kukitezeya

   

Basi haya ni mauti

Walotenda asherati

Lakini kwao laiti

Milele wamejutiya

   

Walitenda pasi haya

Dini kutotegemeya

Ya Mola kuyachezeya

Pasi nyuma kurejeya

   

Yapasa tuyalilie

Mauti yake Husseini

Islamu natulie

Kwa kifo chake Husseini

   

Hapa napenda kukoma

Hadithie kuisoma

Bali mengi sikusema

Dhiki nikiisikiya

   

Kisomoni waungwana

Majumbani na vijana

Mpate jua maana

Mambo yaliyo tukiya

   

Yatupasa Isilamu

Machozi hadi ya damu

Kumliliya Imamu

Kwetu imetupasiya

   

Rabi atamtukuza

Peponi kum-bakiza

Kuzidi akimjaza

Neema kumshushiya

   

Hapa naweka kalamu

Nimefikiya makamu

Wala mbele siyo tamu

Hapa nitakomeleya

YAPASA TUYALILIE MAUTI YAKE HUSSEIN

Na: Masoud Abdallali Muh'd,
Mombasa - Kenya

 

IMAM SHAFII ASEMA:

  1. Hussein! aliuliwa shidi pasi na makosa yoyote na kanzu yake ikatapakazwa wekundu.
  2. Ikiwa dhambi zangu ni kuwapenda watoto wa Mtume Mohammad (s.a.w.) basi ni dhambi ambazo sitatubiya.
  3. Kwa sababu ya Ahlil-Beit wa Mtume (s.a.w.) Ulimwengu mzima ulitetema na majabali na milima ilikaribia kuyeyuka.
  4. Ni nani atakayemfikishia Hussein ujumbe wangu na hata kama nyoyo zatukia?