Subject Index 
Search
Announcements
Feedback
YA SAYYIDNA HUSEINI

Kukuomba sina budi

Ya razaku ya wadudi

Ili utimu mradi

Yote nalo kusudia

   

Sikutaka kusimama

Mengi mno kuyasema

Ni mambo kunisukuma

Ni lazima kuelezea

   

Natokeza hadharani

Kwa ufupi nibaini

Yalomfika Husseini

Ya Rabbi niafikia

   

Yale ni mambo adhimu

Yalomfika Imamu

Sina shaka mwafahamu

Nami tawahadithia

   

Ule mwaka wa sitini

Wahijira sikiani

Kaondoka duniani

Muawiya kajifiya

   

Yazidi alitangaza

Nchi zote kaeneza

Dini ataiongoza

Ili watu kumbaiya

   

Barua aliandika

Madina kaipeleka

Kwa walioikafika

Nae akimwelezea

   

Kwa makini isomeni

Mfahamu yalo ndani

Kahitaji kura zenu

Isilamu wote pia

   

Nazidi kuyabaini

Yalio mwangu moyoni

Ni kura yake Husseini

Ufike kumwelezea

   

Husseini kastakimu

Akasema yakatimu

Huyo ni mtu dhwalimu

Kidini hakutimiya

   

Kama mimi ni haramu

Kukubali ya dhwalimu

Sitaki wake msemu

Mwambiye sitoridhia

   

Kwanza yeye nakiburi

Ni mlevi hana siri

Kajaa kila fujuri

Nyote mnamtambua

   

Sitokuwa chini yake

Hapa na pale afike

Taji hilo silo lake

Hata yeye yamwelea

   

Mtume alibaini

Kwa Hassani na Husseini

Ni Maimamu yakini

Kila mtu kasikia

   

Alifu kumi na mbili

Barua ziliwasili

Kwa mjukue Rasuli

Iraq Zilitokea

   

Barua Zilimtaka

Husseini huko kufika

Ukhalifa kuushika

Dini kuisimamia

   

Yazidi si mtu mwema

Sisi sote twafahamia

Na haya tunayosema

Wewe twakushtakia

   

Husseini hakutwawili

Katuma lbn Akili

Ili kujua ukweli

Wa mambo yalomfikiya

   

Alipokewa vizuri

Wadogo hatakibari

Walimfanya safiri

Wa Husseini Msifiwa

   

Kisha mambo ligeuka

Balozi walimwepuka

Mapanga wakayashika

Muslimu kumuwa

   

Mwezi nane kutimia

Mfungo tatu sikia

Husseini kashika njia

Iraqi kaelekea

   

Naswaha zilimfika

Twakuomba kutotoka

Iraqi usije fika

Watu wakakukimbia

   

Husseini aliwambiya

Hayo yote nasikia

Nitakwenda nadhuria

Mtume kani uswiya

   

Wakiniuwa sijali

Aliniambiya Rasuli

Kua hayo majangili

Dhulima watatumia

   

Alipofika njiani

Ilimaka yakini

Ni hayuko duniani

Muslim kauwawa

   

Iraq waligeuka

Unafiki wakashika

Hivi waja kukushika

Husseini aliambiwa

   

Ule msiba adhimu

Ulomfika Imamu

Yeye na wake kaumu

Nakizaziche pamoja

   

Hapa ni pahali gani

Niambiyeni jamani

Ni Karbala jangwani

Huseini aliambiwa

   

Ibn Saad Omari

Najeshile waliswiri

Maudhi na ujeuri

Imamu wamfanyia

   

Unyama walifanyiwa

Na kiu iliwauwa

Na maji kuzuiliwa

Hayo yote watendewa

   

Kauwawa Akbari

Pia hata Asghari

Na hao watu mashari

Mungu yuwashuhudia

   

Asghari ni kijana

Ni mdogo tena sana

Na kiu ilimbana

Kwa chembe walimuua

   

Husseini aliuuiiza

Fikirini mukiwaza

Kosa gani tulifanza

Kutendewa kama haya

   

Himambo yenye huzuni

Alotendewa Husseini

Nashindwa kuyabaini

Ukumbuni ngatokea

   

Yangu haki mumetwaa

Ya ukhalifa sisawa

Na leo mwanisumbua

Nilipi mwafikiria

   

Au hamkusikia

Usemi wahashimia

Hapo akiwauswia

Kuhusu wake dhuria

   

Mama yangu ni Batuli

Binti yake Rasuli

Na baba yangu ni Ali

Waswii wake Nabia

   

Ya Husseini walimwaga

Damu yake bila woga

Walijifanya wajinga

Ufasiki mewashika

   

Kijukuu cha Rasuli

Ni Husseini bin Ali

Achinjwa kama ghazali

Wallahi twakulilia

   

Alipewa kila dhuli

Mwanao ewe Batuli

Ateswa na majangili

Waso dini sikiya

   

Walisahau ahadi

Ya Mtume Muhammadi

Na wote ni mashahidi

Mtume akiwauswia

   

Alimchinja Husseini

Bila khofu na huzuni

Na Mungu si Athumani

Nae atamlipia

   

Ni kifo chenye kutisha

Tena kina babaisha

Wallahi chahuzunisha

Kila kinapo tolewa

   

Na Mungu si Athmani

Twalipa duniani

Wa kesho wenda motoni

Adhabu yawangojea

   

Hapo ndipo nitafika

Kalamu chini naweka

Kwa huzuni lonishika

Siwezi kuendelea

   

Mola atupe Imani

Yakumpenda Husseini

Tuwe nae na peponi

Dua zetu zipokea

   

Kisha Swala na Salamu

Zende hadi kwa Hashimu

Na alize Mainwnu

Hasidi angachukia