34. Katika Tawba Ulimi Ndiyo Mfasiri Wa Moyo
Katika TAWBA, kama tulivyokwisha elezea hapo awali kuwa kitu cha lazima ni kusikitika na kuhuzunika kwa mtu, vile vile kujuta kwa moyo wake wote pamoja na kunuia kwake kuacha madhambi hayo na yote mengineyo. Na katika hisia hizo nzito atamke maneno mazito ya kuomba msamaha wa Allah swt na kusema: 'Astaghfirullah Rabbi wa atubu Ilayhi.'
TAWBA haiwezi kuwa TAWBA iwapo itatamkwa mdomoni tu bila ya kuwapo kwa hisia za moyoni. Hivyo inatubidi tuuelekeze ulimi wetu katika TAWBA baada ya kujengwa kwa hisia za moyoni kwani ulimi ndio utakao fasiri yaliyo moyoni mwetu. Ndipo hapo TAWBA yetu itakuwa ni sahihi.
Mfano, ninajuta na kusikitika kwa kusema matusi na maneno machafu moyoni mwangu, lakini ulimi wangu bado unaendelea na kuyasema hayo hayo. Basi katika hali kama hii, ulimi haujawa mfasiri wa moyo wangu. Utakuwa mfasiri pale utakapoacha kuyasema maneno hayo na mengineyo pia.
Hivyo tuombe Tawfiki ya kujaaliwa ulimi wetu uwe mfasiri wa moyo wetu ili kutukamilishia TAWBA kimoyo na kimatendo. Vile vile juhudi zetu pia zinahitajika, katika kujielekeza huko.
Ipo hadithi Tukufu isemayo:
"Adda'i bila Aamal kar-raami bila watr" Yaani:
Mwombaji bila matendo ni sawa na upinde bila kamba yake, au mti bila matunda, au mto bila maji.
Sasa tujiulize iwapo tutaomba tu bila kujitahidi wenyewe itakuwaje?