read

37. Mazungumzo Ya Imam Zaynul Aabediin Na Zahra

Imam Zaynul Aabediin a.s. alikuwa akielekea Makkah na aliliweka hema lake chini ya mlima mmoja ujulikanao kama 'Zahra.' Zahra alikuwa ni hakimu na pia alikuwa mfuasi wa Imam Zaynul Aabediin a.s. na alikuwa akimtembelea mara kwa mara.

Huyo Zahra siku moja alimhukumu mtu mmoja kifungo kwa makosa aliyokuwa ameyatenda, na kwa bahati mbaya huyo mfungwa alifariki akiwa kifungoni. Kutokana na tukio hilo, Zahra alijitoa hapo mjini Madina na kuishi katika mlima huo huu akilia na kujuta mno akiwa amewaacha mke na watoto wake wote.

Imam a.s. aliambiwa, "Zahra amevunjika moyo na kuwehuka na yupo daima akilia tu. Je, utapendelea kuonana naye kwani alikuwa ni miongoni mwa wakupendao wewe? Na Imam a.s. aliwajibu kuwa angelipendelea kumwona na kujua hali yake.

Hapo Imam a.s. alimwendea huyo Zahra mlimani kwa kutaka kumpa mawaidha na hidaya. Zahra alikuwa uchi na katika hali ya kulia tu na alikuwa amedhoofika kabisa.

Riwaya inaendelea kusema kuwa Imam a.s. alimwambia: "Kutotegemea na kutarajia rehema na Maghfrrah za Allah swt kwenyewe ni dhambi mojawapo kuu hata kuliko tendo lako ulilolifanya. Sasa kwa nini hutaki kujitafutia njia ya kupona na hayo."

Hapo Zahra alijikaza na kusema, "Ewe bwana, je kunawezekana kukapatikana njia ya kuniponya na hayo niliyokuwa nimeyatenda kwani mimi nilimwua mtu katika hukumu yangu!"

Hapo Imam a.s. alimwambia: "Nenda kwa jamaa zake uwafidie na kuwaomba msamaha na urejee katika kazi yako hiyo hiyo kwani itakuwa na manufaa kwako humu duniani na akhera pia. Je, humu duniani kuna maumivu yoyote yale yasiyoweza kupatiwa ufumbuzi na matibabu yake? Inambidi kila mtu afanye haraka ya kufanya TAWBA na hii ndiyo njia ya kujipatia msamaha na rehema za Allah swt kwa haraka na urahisi wenye uhakika."

Njooni leo tufanye TAWBA kwa madhambi yote tuliyokwisha tenda na tunuie kutotenda tena madhambi yoyote yale.Tufanye TAWBA leo kwani mauti haina wakati.