41. Tawba Hutuepusha Na Moto Wa Jahannam
Imam Jaafer as-Sadique a.s. amenakiliwa riwaya moja katika Usuli Kaafi:
Siku moja Imam Ali ibn Abi Talib a.s. alimtembelea Sahaba mmoja na hapo alitokezea mtu mmoja akisema: "Ya Ali! Mimi nimetenda tendo la aibu pamoja na kijana mmoja (ulawiti), hivyo naomba nitakasike kwa mujibu wa Shariah za Allah swt."
Imam Ali a.s. alimwambia:"Kwa hivi sasa naomba uende zako kwani inawezekana ulitenda tendo hilo kwa ushawishi uliokuwa umekughalibuNa hivyo inawezekana kuwa akili zako hazikuwa timamu na maneno yako yasiwe yenye fahamu au maana yoyote."
Huyo mtu alirijea siku ya pili na kuyasema yale yale tena ya kutaka aadhibiwe.
Kwa mara ya pili, Imam Ali a.s. "alimwambia kuwa labda ulitenda katika hali ya ghadhabu ambayo ilikughlibu."
Aliporudia mara ya nne, Imam Ali a.s. alimwambia: "Mtume Mtukufu s.a.w.w. alitoa hukumu tatu katika sura kama hii, hivyo uchague mojawapo unayoipenda: (1) mikono na miguu yako ifungwe kwa pamoja na wewe utupwe chini kutoka mlimani, (2) Kichwa chako kikatwe kwa upanga na (3) Uchomwe mzima mzima kwa moto."
Hapo huyo mtu akamwuliza Imam Ali a.s..,"Je, ni adhabu ipi iliyo ngumu kati ya hizo tatu?" Na Imam Ali a.s. alimjibu, "Adhabu ya kuchomwa kwa moto." Na hapo huyo mtu alichagua kuchomwa kwa moto. Na alisema kuwa yu tayari kwa hayo.
Baada ya hapo aliondika, akaenda kusali rakaa mbili na akaanza kusema: "Ewe Allah swt! Mimi nilishawishiwa na hisia zangu za kinyama na dhamira yangu ipo ikinilaumu, nami ninaogopa madhambi na hivyo nimejileta mbele ya Mpenzi wa Mtume wako Muhammad s.a.w.w. ili yeye aniadhibu vilivyo kwa makosa yangu. Yeye amenielezea kuwa kuna adhabu tatu, nami, Ewe Allah swt! nimechagua ile ambayo ni ngumu kuliko zinginezo na ni matumaini yangu kuwa wewe U mkarimu na mrehemavu basi utanisamehe madhambi yangu kwa adhabu yangu hiyo ikiwa ni kaffar na utaniepusha na Moto wa Jahannam na ghadhabu zako."
Baada ya hapo alilia mno na kujielekeza katika moto. Miale ya moto yaliongezeka. Hapo Imam Ali a.s. pamoja na Sahaba wake walipoona hali hiyo, walilia mno. Na Imam Ali a.s. alisema: "Ewe mtu! Inuka, wewe umewaliza hata Malaika wa ardhini na mbinguni,yakini TAWBA yako imekubaliwa mbele ya Allah swt!"
Imam Jaafer as-Sadique a.s. amenakiliwa katika Bihar al-Anwaar cha Allamah Majlisi A.R. hivi:
Zipo mashua mbili zikielea majini mojawapo ipo imepakia shehena ya bidhaa na nyingine ipo tupu. Zinakaribia bandari ya nchi fulani na huko wanawakuta Maofisa forodha na kodi wakiwasubiri kupakua na kukisia kodi ya kuwatoza.
Je, mashua ipi itakayopita upesi bila ya kuulizwa maswali mengi na kufanyiwa upekuzi mkali? Bila shaka ni ile mashua isiyo na shehena ya bidhaa.
Mashua yenye shehena ya bidhaa itapekuliwa na kuhojiwa maswali mengi ya kila aina na bila shaka itachukua muda mrefu sana kabla haijaruhusiwa kuendelea na shughuli yake na kufika katika manxili yake. Na hapo watalipizwa kodi kubwa bila shaka na labda kupewa adhabu kali iwapo kutatokea hali isiyo halali.
Vivyo hivyo iwapo mtu atakufa huku akiwa ameshajitakasisha kwa kutimiza wajibu wake TAWBA basi siku ya Kiyama hatakuwa na muda mrefu wa kuhojiwa kwani atakuwa ametimiza wajibu wake humu duniani sala, zaka, khusi, saumu n.k. na vile vile amekuwa akiwatunza ahali yake, hakuwadhulumu wala kuwaonea watu, wazazi wake wamekuwa daima wakiangaliwa naye na kutimiza haki zao vile vile majirani wake na majamaa wake pia wamekuwa wakiangaliwa naye. Yaani kwa ufupi, amekuwa ni mwislamu mwenye kuzingatia maamrisho ya Allah swt wakati akiwa yu hai humu duniani. Basi mtu kama huyo hatakuwa na mengi ya kuulizwa wala shida yoyote katika safari yake hiyo.
Vile vile ipo riwaya nyingineyo isemayo mtu kama huyo atakapoteremshwa kaburini kutakuwa kumejawa na nuru na atakuta kuna msafirishaji wake hapo na katika punde atajikuta yupo Jannati (peponi). Hapo wakazi wa Paradiso watamwuliza "Je, vipi mambo yako ya maswali na majibu yamekwendaje?" Na jee usafiri huu vipi? Basi hapo huyo atajibu: "Huu usafiri ni msikiti ambao nilikuwa nikiupenda mno nilipokuwa duniani na sasa umenifikisha hadi hapa Peponi."
Tuelewe wazi wazi kuwa Maasumiin-min -Allah ni shakhsiyyah wasiyo kuwa na madhambi na vile vile wale ambao watatenda mema na kufanya TAWBA ni sawa na watu wasiopata kutenda madhambi kamwe, hivyo ndivyo isemavyo Quran Tukufu na riwaya mbali mbali.
Na Allah swt amewaahidi watu kama hao: Sura al-Furqaan:
...Hao (waliotubia) ndio Mwenyezi Mungu atawabadilishia maovu yao kuwa mema.........(25:70)
Kwa kifupi ni kwamba iwapo mtu atafariki dunia akiwa hana dhambi basi hatakuwa na maswali mengi ya kuulizwa na wala hatasumbuliwa popote pale katika safari yake hiyo. Iwapo mtu atakuwa amejitwisha mzigo mzito wa madhambi, basi atakuta maswali na mahojiano mengi yakimsubiri kwa muda mrefu katika Barzakh hadi hapo atakapotakasika kabisa na kuingia katika siku ya Kiyama.
Al-Imam as-Sadique a.s. amenakiliwa riwaya: "Mtu yeyote ampendaye Ali a.s. na kuwachukia maadui wake, na iwapo atakuwa amejitwisha mzigo wa madhambi bila TAWBA, basi huyo atabakia muda mrefu katika Barzakh akiadhibiwa hadi kutakasika kabisa. Atakapotokea siku ya malipo atakuwa hana la kujibu kwani atakuwa ametakasika."
(Tafsir Nuru Thaqalain, Kitabu cha tano, Uk. 165: Tafsir Majmaul Bayaan).
Imam a.s. alisema vile vile: "Mimi ninawakhofia mno adhabu za Barzakh (kizuizi) na siku ya kiyama tutawatetea waumini."
Hivyo inatubidi sisi tufanye TAWBA sahihi na kamilifu kabla ya kifo chetu ili tukifa tuwe ni waumini wa kweli ndipo tutakapopatiwa Shifaa ya Mtume s.a.w.w. na Maimamu a.s. kwani sisi tulivyo dhaifu hatutaweza kustahimili adhabu za mwenyezi Mungu na moto wa Jahannam. Tuelewe vyema kuwa huwa daima mauti inatufuata kama vile kilivyo kivuli chetu na labda muda huu tulio nao ndio wa mwisho, hivyo TAWBA ndiyo suluhisho letu la kuokoka humu duniani na vile vile Aakhera.