read

Aya 27 – 31: Kila Umma Utaitwa Kwenye Kitabu Chake

Maana

Na ufalme wa mbingu na ardhi ni wa Mwenyezi Mungu.

Mwenyezi Mungu anaashiria, kwa kauli hii, kwamba aliyeumba mbingu na ardhi na wala asichoke, bila shaka, ni muweza wa kuhuisha wafu.

Na siku itaposimama Saa ya Kiyama, siku hiyo watahasirika wenye batili, kwa sababu makazi yao ni motoni siku hiyo, wala hawatakuwa na wa kuwasaidia.

Na utauona kila umma umepiga magoti.

Mwenyezi Mungu (s.w.t.) atawafufua watu wakiwa wamepiga magoti wakingoja hisabu na malipo. Sio mbali kuwa hiki ni kinaya cha fazaa na hofu itakayojitokeza.

Kila umma utaitwa kwenye kitabu chake: Leo mtalipwa mliyokuwa mkiyatenda.

Makusudio ya kitabu hapa ni maandishi ya matendo. Maana ni kuwa kila umma na kila mtu atalipwa kwa aliyoyatenda. Kwenye Nahjul-balagha, Imam Ali (a.s.) anasema: “Anapokufa mtu watu husema alichokiacha, na Malaika husema alichokileta”

Hiki kitabu chetu kinasema juu yenu kwa haki. Hakika Sisi tulikuwa tukiyaandika mliyokuwa mkiyatenda.

Kesho wakosefu wataambiwa haya ndiyo tuliyoyaandika kuhusiana na nyinyi. Picha kamili ya matendo haina nyongeza wala upungufu. Kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwaamrisha Malaika kusajili vitendo vyenu na kuvihifadhi kwa pumzi zenu mlizozitumia kwenye maasi.

وَيُنْذِرَ الَّذِينَ قَالُوا اتَّخَذَ اللَّهُ وَلَدًا {4}

“Ole wetu! Kina nini kitabu hiki hakiachi dogo wala kubwa ila kinalihesabu? Na watakuta waliyoyafanya yamehudhurishwa. Na Mola wako hadhulumu yoyote.” Juz. 15 (18:4).

Ama wale walioamini na wakatenda mema, Mola wao atawaingiza katika rehema yake. Huko ndiko kufuzu kulio wazi.

Walifuata njia ya amani, Mwenyezi Mungu akawaongoza katika rehema yake. Imam Ali (a.s.) anasema: “Hatafuzu kwa heri ila mwenye kuifanyia kazi, wala hatafedheheka na shari ila aliyeifanya.”

Na ama wale waliokufuru, wataambiwa: Kwani hamkuwa mkisomewa Aya zangu nanyi mkawa na kiburi, na mkawa watu wakosefu?

Kesho Mwenyezi Mungu (s.w.t.) atawambia waasi waliokuwa na inadi na kiburi, kwa kuwasuta na kuwatahayariza kuwa mliisikia sauti ya haki hamkuitika na mkaona dalili waziwazi mkazipinga kwa inadi na kiburi; mkastarehe kwenye ufisadi na upotevu, basi leo nyinyi ni katika waliohasirika.

وَإِذَا قِيلَ إِنَّ وَعْدَ اللَّهِ حَقٌّ وَالسَّاعَةُ لَا رَيْبَ فِيهَا قُلْتُمْ مَا نَدْرِي مَا السَّاعَةُ إِنْ نَظُنُّ إِلَّا ظَنًّا وَمَا نَحْنُ بِمُسْتَيْقِنِينَ {32}

Na ikisemwa: Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli, na Saa haina shaka, nyinyi mkisema: Hatuijui hiyo Saa, tunadhania dhana tu, wala hatuna yakini.

وَبَدَا لَهُمْ سَيِّئَاتُ مَا عَمِلُوا وَحَاقَ بِهِمْ مَا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ {33}

Na ubaya wa waliyoyatenda utawadhihirikia, na yatawazunguka waliyokuwa wakiyafanyia mzaha.

وَقِيلَ الْيَوْمَ نَنْسَاكُمْ كَمَا نَسِيتُمْ لِقَاءَ يَوْمِكُمْ هَٰذَا وَمَأْوَاكُمُ النَّارُ وَمَا لَكُمْ مِنْ نَاصِرِينَ {34}

Na itasemwa: Leo tunawasahau kama mlivyosahau mkutano wa siku yenu hii; na mahali penu ni Motoni, wala hamna wa kuwanusuru.

ذَٰلِكُمْ بِأَنَّكُمُ اتَّخَذْتُمْ آيَاتِ اللَّهِ هُزُوًا وَغَرَّتْكُمُ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا ۚ فَالْيَوْمَ لَا يُخْرَجُونَ مِنْهَا وَلَا هُمْ يُسْتَعْتَبُونَ {35}

Hiyo ni kwa sababu nyinyi mlizifanyia mzaha Aya za Mwenyezi Mungu; na maisha ya dunia yakawadanganya. Basi leo hawatatolewa humo wala hao hawatakubaliwa udhuru.

فَلِلَّهِ الْحَمْدُ رَبِّ السَّمَاوَاتِ وَرَبِّ الْأَرْضِ رَبِّ الْعَالَمِينَ {36}

Basi sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa mbingu, na Mola wa ardhi, na Mola wa walimwengu wote.

وَلَهُ الْكِبْرِيَاءُ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۖ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ {37}

Na ukubwa ni wake, mbinguni na katika ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.