read

Aya 7 – 10: Wanaobeba Arshi

Maana

Wale wanaobeba Arshi, na wanaoizunguka, wanamsabihi na kumsifu Mola wao, na wanamuamini.

Katika Juz. 8 (7:54), tulisema kuwa makusudio ya kuwa kwenye Arshi ni kutawala. Na katika Aya ya 75 ya sura iliyopita, tukasema kuwa makusudio ya Malaika kuizunguka Arshi ni kuwa hawamtangulii Mwenyezi Mungu kwa kauli na wanafanya kwa amri yake. Nasi tuna mategemeo kuwa kauli yetu hii, kwa kulinganisha na mfumo wa maneno, inaendana na tafsiri hii.
Ama mfumo wa Aya hii tuliyo nayo na ile inayosema: “Na wanane juu ya wao watachukua Arshi ya Mola wako” (69:17) unatufanya tutafute maana nyingine ya Arshi inayochukuliwa; ingawaje kuchukua Malaika Arshi hakulazimishi kuwa Mungu amekaa juu yake.

Ikiwa hivyo basi itabidi Mwenyezi Mungu awe ana mwili na pia awe yuko mahali fulani na kwengine hayuko. Ikiwa utauliza: Kama Mwenyezi Mungu hakukaa katika Arshi (kiti cha enzi), kwa nini basi ikanasibishwa kwake, na kusemwa ‘Arshi ya Mola wako.’

Jibu: suala la kunasibisha ni la kawaida na jepesi sana; kwa mfano inaweza kuitwa barabara ya fulani, wakati huyo fulani mwenyewe hata haijui barabara hiyo; sembuse muumba wa ulimwengu wote? Majumba yote ya kuabudu mashariki na magharibi, sikwambii Al-Kaaba tukufu, yanaitwa ni ya Mwenyezi Mungu. Je, hiyo inamaanisha kuwa Mwenyezi Mungu anaishi humo?

Inawezekana kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ametengeneza Arshi na kuamrisha Malaika wake waizunguke; kama alivyomwamrisha Ibrahim kujenga nyumba kongwe na kulazimisha kuizuru na kuizunguka kila mwenye kuweza kuifika.

Vyovyote iwavyo ni kuwa Malaika wanamwamini Mwenyezi Mungu na kumtukuza kwa kumsifu na wanawaombea msamaha walio amini kwa kusema: Mola wetu! Umekienea kila kitu kwa rehema na ujuzi. Basi wasamehe ambao wametubu na wakaifuata Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu.

Waumini wenye ikhlasi wana aina nyingi ya malipo; zikiwemo Bustani zinazopitiwa na mito chini yake, kuwa marafiki wa manabii na mashahidi na kwamba Malaika wanawatukuza kwa kuwasifu na kuwaombea Mungu wawe na daraja ya juu na kukingwa na ghadhabu yake na adhabu yake.

Mola wetu! Na waingize katika Bustani za Milele ulizowaahidi. Na pia waliofanya mema miongoni mwa wazee wao na wake zao na dhuriya zao. Hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Malaika watamuomba Mwenyezi Mungu kesho awakusanye familia kwenye Pepo yake; kama walivyokuwa duniani ili wazidi kuwa na furaha. Kauli yake: ‘waliofanya mema,’ inaashiria kukatika udugu baina ya mumin na kafiri, hata kama mmoja ni baba wa mwingine;

فَإِذَا نُفِخَ فِي الصُّورِ فَلَا أَنْسَابَ بَيْنَهُمْ يَوْمَئِذٍ {101}

“Basi itakapopuziwa parapanda, hapo hakutakuwa na nasaba baina yao.” Juz. 18 (23:101).

الْأَخِلَّاءُ يَوْمَئِذٍ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ عَدُوٌّ إِلَّا الْمُتَّقِينَ {67}

“Siku hiyo marafiki watakuwa maadui wao kwa wao isipokuwa wenye takua” (43:67).

Na waepushe na maovu; kwani umwepushaye maovu siku hiyo, hakika umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.

Wakinge na kila ubaya siku ya kiyama. Hakuna mwenye shaka kwamba mwenye kupata daraja hii mbele ya Mwenyezi Mungu atakuwa amefuzu fadhila zake na rehema zake.

Kwa hakika wale waliokufuru watanadiwa: Bila ya shaka kuchukia Mwenyezi Mungu ni kukubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu, mlipokuwa mnaitwa kwenye imani mkakataa.

Watu wa motoni watachukia wakiwa humo ndani kutokana na yaliyowaleta humo. Huko duniani walikuwa wakiyapenda na kuyaridhia. Mwito utawajia huku wakijilaani wenyewe kuwa, alivyokuwa Mwenyezi Mungu akichukia kufuru yenu duniani ni zaidi sana ya mnavyojichukia nyinyi hivi sasa. Mwenyezi Mungu (s.w.t.) aliwalingani kupitia mitume wake, lakini mkakataa isipokuwa ukafiri. Basi onjeni adhabu leo, na madhalimu hawana msaidizi.

قَالُوا رَبَّنَا أَمَتَّنَا اثْنَتَيْنِ وَأَحْيَيْتَنَا اثْنَتَيْنِ فَاعْتَرَفْنَا بِذُنُوبِنَا فَهَلْ إِلَىٰ خُرُوجٍ مِنْ سَبِيلٍ {11}

Watasema: Mola wetu! Umetufisha mara mbili, na umetuhuisha mara mbili! Basi tunakiri madhambi yetu. Basi je, ipo njia ya kutoka?

ذَٰلِكُمْ بِأَنَّهُ إِذَا دُعِيَ اللَّهُ وَحْدَهُ كَفَرْتُمْ ۖ وَإِنْ يُشْرَكْ بِهِ تُؤْمِنُوا ۚ فَالْحُكْمُ لِلَّهِ الْعَلِيِّ الْكَبِيرِ {12}

Hayo ni kwa sababu alipoombwa Mwenyezi Mungu peke yake mlikataa. Na akishirikishwa mnaamini. Basi hukumu ni ya Mwenyezi Mungu Mtukufu Mkubwa.

هُوَ الَّذِي يُرِيكُمْ آيَاتِهِ وَيُنَزِّلُ لَكُمْ مِنَ السَّمَاءِ رِزْقًا ۚ وَمَا يَتَذَكَّرُ إِلَّا مَنْ يُنِيبُ {13}

Yeye ndiye ambaye anawaonyesha Ishara zake, na anawateremshia riziki kutoka mbinguni. Na hapana anayekumbuka ila anaye rejea.

فَادْعُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ {14}

Basi mwombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye, wajapochukia makafiri.

رَفِيعُ الدَّرَجَاتِ ذُو الْعَرْشِ يُلْقِي الرُّوحَ مِنْ أَمْرِهِ عَلَىٰ مَنْ يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ لِيُنْذِرَ يَوْمَ التَّلَاقِ {15}

Ndiye Mwenye daraja za juu. Mwenye Arshi. Hupeleka Roho, kwa amri yake, juu ya amtakaye katika waja wake, ili kuonya Siku ya kukutana.

يَوْمَ هُمْ بَارِزُونَ ۖ لَا يَخْفَىٰ عَلَى اللَّهِ مِنْهُمْ شَيْءٌ ۚ لِمَنِ الْمُلْكُ الْيَوْمَ ۖ لِلَّهِ الْوَاحِدِ الْقَهَّارِ {16}

Siku watakayodhihiri wao. Hapana kitachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu Mmoja Mtenza nguvu.

الْيَوْمَ تُجْزَىٰ كُلُّ نَفْسٍ بِمَا كَسَبَتْ ۚ لَا ظُلْمَ الْيَوْمَ ۚ إِنَّ اللَّهَ سَرِيعُ الْحِسَابِ {17}

Leo kila nafsi italipwa kwa iliyoyachuma. Hapana dhulma leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.