read

Aya 6-10: Kuapizana Mume Na Mke

Maana

Katika vitabu vya Fiqh kuna mlango unaoitwa Lian, ambao chimbuko lake ni Aya hizi. Inafanana na kuapizana baina ya mume anayemtuhumu mkewe na zina bila ya kuwa na ushahidi wa madai yake, na mke kuikana tuhuma ya zina yeye mwenyewe. Lengo la kulaniana huku ni kuondoka adhabu ya kutuhumu au kumkana mtoto. Liani haiwi ila katika hali mbili:

Kwanza: Mtu kumtuhumu na zina mkewe wa kisharia aliyemuoa kwa ndoa ya daima. Ni lazima mke awe si kiziwi wala bubu, mume adai kushuhudia na asiwe na ubainifu wa kisharia juu ya hiyo zina, zikikosekana sharti hizi basi haijuzu kulaniana.

Pili: Kumkana mume mtoto wa kitanda chake, ikiwa mimba haikupungua miezi sita au kuzidi mwaka. Vinginevyo anaweza kumkana mtoto bila ya kulaniana.

Basi ikiwa mume atamtuhumu mkewe na zina au kumkana mtoto,anatakikana apate adhabu (had) ya kutukana, ila akileta ushahidi au kulaniana.

Sura ya kulaniana ni kusema mbele ya hakimu wa sharia: Ninashuduia kuwa mimi ni mkweli kwa ninayoyasema kuhusu mke wangu fulani. Atasema hivyo mara nne; kisha atasema mara ya tano baada ya kuonywa na hakimu wa sharia: Laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yangu ikiwa ni muongo.

Mke naye atashuhudia mara nne kwamba huyo mume ni muongo kwa aliyomtuhumu nayo. Mara ya tano atasema ghadhabu za Mwenyezi Mungu zimshukie ikiwa huyo mume ni mkweli.

Ni lazima wote wawili wawe wamekaa wakati wa kulaniana. Kukishatimia kulaniana kwa masharti yake, matokeo yatakuwa ni mambo yafuatayo:-

1. Ndoa itavunjika.

2. Uharamu wa milele baina ya mume na mke (hawawezi kurudiana tena).

3. Adhabu ya kutuhumu itaondoka kwa mume.

4. Mtoto hatakuwa wa mume. Hawatarithiana wala halazimiki kumtunza. Lakini atakuwa ni wa mama kisharia.

Tukijua kulaniana baina ya mume na mke, itakuwa tumejua makusudio ya Aya hizi. Kwa hiyo basi tutafupiliza kufasiri kwa kutaja matamko yanayoashiriwa na mfumo wa maneno.

Na wale wanaowasingizia wake zao kwa zina na hawana mashahidi ila nafsi zao kutokana na madai yao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa kushuhudia mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu ya kwamba hakika yeye ni katika wasema kweli.

Atayasema hayo mbele ya hakimu wa sharia.
Na mara ya tano kwamba laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa ni miongoni mwa waongo.

Yaani ikiwa ni muongo katika madai yake. Na mke itamwondokea adhabu kwa kutoa shahada mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu, kwamba huyo mume ni miongoni mwa waongo. Mke naye atatoa ushahidi wake mbele ya hakimu wa sharia kama alivyofanya mume.

Na mara ya tano kwamba ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake, kama mume ni miongoni mwa wasemao kweli katika haya madai yake kwangu.

Na lau kuwa si fadhila za Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake mngeliangamia.

Na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye kutakabali, toba Mwenye hekima.

Hii ni kuashria hekima ya sharia ya kuapizana, kwamba lengo ni kusitiri na kuondoa adhabu kwa mume na kutoa nafasi kwa mke kujitetea na tuhumu za mume.

إِنَّ الَّذِينَ جَاءُوا بِالْإِفْكِ عُصْبَةٌ مِنْكُمْ ۚ لَا تَحْسَبُوهُ شَرًّا لَكُمْ ۖ بَلْ هُوَ خَيْرٌ لَكُمْ ۚ لِكُلِّ امْرِئٍ مِنْهُمْ مَا اكْتَسَبَ مِنَ الْإِثْمِ ۚ وَالَّذِي تَوَلَّىٰ كِبْرَهُ مِنْهُمْ لَهُ عَذَابٌ عَظِيمٌ {11}

Hakika wale walioleta uzushi ni kundi miongoni mwenu. Msiufikirie ni shari kwenu, bali hiyo ni kheri kwenu. Kila mmoja katika wao atapata aliyoyachuma katika madhambi. Na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao atapata adhabu kubwa.

لَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ ظَنَّ الْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بِأَنْفُسِهِمْ خَيْرًا وَقَالُوا هَٰذَا إِفْكٌ مُبِينٌ {12}

Mbona mlipousikia, waumini wanaume na waumini wanawake hawakujidhania mema na kusema huu ni uzushi dhahiri?

لَوْلَا جَاءُوا عَلَيْهِ بِأَرْبَعَةِ شُهَدَاءَ ۚ فَإِذْ لَمْ يَأْتُوا بِالشُّهَدَاءِ فَأُولَٰئِكَ عِنْدَ اللَّهِ هُمُ الْكَاذِبُونَ {13}

Mbona hawakuleta mashahidi wane. Na kwa kutoleta mashahidi, basi hao mbele ya Mwenyezi Mungu ni waongo

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ لَمَسَّكُمْ فِي مَا أَفَضْتُمْ فِيهِ عَذَابٌ عَظِيمٌ {14}

Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake katika dunia na akhera, bila shaka ingeliwapata adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyojiingiza.

إِذْ تَلَقَّوْنَهُ بِأَلْسِنَتِكُمْ وَتَقُولُونَ بِأَفْوَاهِكُمْ مَا لَيْسَ لَكُمْ بِهِ عِلْمٌ وَتَحْسَبُونَهُ هَيِّنًا وَهُوَ عِنْدَ اللَّهِ عَظِيمٌ {15}

Mlipoyapokea kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyoyajua, na mkifikiri ni dogo kumbe kwa Mwenyezi Mungu ni kubwa.

وَلَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ قُلْتُمْ مَا يَكُونُ لَنَا أَنْ نَتَكَلَّمَ بِهَٰذَا سُبْحَانَكَ هَٰذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ {16}

Na mbona mliposikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya; utakatifu ni wako! Huu ni uzushi mkubwa.

يَعِظُكُمُ اللَّهُ أَنْ تَعُودُوا لِمِثْلِهِ أَبَدًا إِنْ كُنْتُمْ مُؤْمِنِينَ {17}

Mwenyezi Mungu anawaonya msirudie kufanya kama haya kabisa ikiwa nyinyi ni waumini.

وَيُبَيِّنُ اللَّهُ لَكُمُ الْآيَاتِ ۚ وَاللَّهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ {18}

Na Mwenyezi Mungu anawabainishia Aya na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

إِنَّ الَّذِينَ يُحِبُّونَ أَنْ تَشِيعَ الْفَاحِشَةُ فِي الَّذِينَ آمَنُوا لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ ۚ وَاللَّهُ يَعْلَمُ وَأَنْتُمْ لَا تَعْلَمُونَ {19}

Hakika wale ambao wanapenda kueneza uchafu kwa waliaomini watapata adhabu chungu duniani na akhera. Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui.

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ وَأَنَّ اللَّهَ رَءُوفٌ رَحِيمٌ {20}

Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake na kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni Mpole, Mwenye kurehemu.