read

Aya 37 – 44: Kila Kitu Kina Ishara

Maana

Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ametaja ishara za ulimwengu zinazofahamisha uweza wake na ukuu wake; kama ifutavyo:

Na usiku ni Ishara kwao. Tunauvua humo mchana, mara wao wanakuwa gizani.

Usiku unafuatana na mchana kutokana na kuwa ardhi ni tufe na kuwa inazunguka kama jiwe la kusagia. Wakati ardhi inapozunguka, upande ule unaolielekea jua unakuwa ni mchana na ule usiolieleka jua unakuwa ni usiku. Nao ukifikia kwenye jua unakuwa mchana na ule mwingine unakuwa usiku, na kuendelea namna hiyo.

Hali hiyo ndiyo aliyoitolea ibara Mwenyezi Mungu (s.w.t.) kuwa ni kuvua. Na amekutegemeza kwake Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t.) kwa sababu ndiye mumba wa ulimwengu na msababishaji wa sababu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 3 (3:27) na Juz. 15 (17:12).

Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Mwenye kujua.

Wafasiri wametofautiana katika makusudio ya neno Mustaqarrin lahaa, tulilolifasiri kwa maana ya kiwango chake. Razi ameishilia kwenye kauli nne, lakini zote ziko mbali na ufahamu. Ilivyo hasa ni kinaya cha kwenda kwa nidhamu na mpangilio.

Hilo linatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu, Mwenye kujua’ Mwandishi wa kitabu Al-qur’an wal-ilmulhadith (Qur’an na sayansi) amenukuu wataalamu wa falaki wa kisasa wakisema: Jua linakwenda kwa kasi ya maili 12 kwa sekunde mbali ya kuwa hilo lenyewe linazunguka, na kwamba linatofautiana na mzunguuko wa ardhi.

Yametangulia maelezo yanayoambatana na haya katika Juz. 13 (13:2).

Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka ukarudi kuwa kama karara la zamani.

Vituo hivi havibadiliki au kuondoka mahali pake, wala mwezi haupotei navyo. Wana falaki wanasema kuwa ni 28. Mwezi unashuka usiku kwenye kila kimoja na unajificha nyusiku mbili ikiwa mwezi utakuwa wa siku 30 na usiku mmoja ukiwa na siku 29.

Wakati huo unakuwa kama tawi la mtende kwa wembamba. Haya ndio makusudioya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘karara.’ Yametangulia yanayofungamana na haya katika Juz.10 (9: 36 – 37) kifungu cha ‘miezi miandamo ndiyo miezi ya kimaumbile’

Haliwi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita mchana. Na vyote vinaogelea katika njia.

Kila sayari ina njia yake maalum, ikizunguka humo kwa nidhamu na kwenda kwenye kituo chake kilichopangiwa mpaka atakapozikunja Mwenyezi Mungu kama karatasi. Kwenye Nahjul-balagh kuna maelezo haya: “Na akalifanya Jua lake – yaani jua na hizo sayari - kuwa ni ishara yenye kuonwa na mchana wake, na Mwezi wake kuwa unaufuta usiku wake; yaani mwangaza wa mwezi unazidi miangaza ya sayari nyinginezo. Basi akazipitisha katika njia yake ili upambanuke usiku na mchana kwazo na ili ijulikane idadi ya miaka na hisabu kwa makisio ya hizo mbili.

Miongoni mwa niliyoyasoma katika maudhui haya ni Hadith Qudsi aliyoitaja mwenye kitabu cha Al-asfar Jalada la tatu, maana yake ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amesema: Lau jua lingewekwa upande maalum, basi matajiri wangelijenga jengo refu kuzuia mwanga wa Jua usiwafikie mafukara, lakini ameliweka kwenye anga likizunguka na kwenda, ili fukara apate sehemu yake, sawa na anavyopata tajiri.

Na ni ishara kwao kwamba tuliwapakia dhuriya zao katika jahazi ilio sheheni.

Kwao, ni kwao hao Binadamu. Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anawakumbusha neema zake kuu kwao; miongoni mwazo ni kuwabeba kwenye majahazi wao na mizigo yao, wakitolewa huku na kupelekwa kule. Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (14:32) na Juz. 15 (17:66).

Na tukawaumbia kutoka mfano wake wanavyovipanda.

Yaani mfano wa majahazi. Wafasiri wa kale walisema kuwa makusudio ya mfano wake ni ngamia, farasi, nyumbu na punda. Walisema haya wakati ambapo hakukuwa na ndege wala gari au chombo chote cha angani.

Na tukitaka tunawagharikisha hata kama wako katika manowari na meli.

Lengo ni kuwakumbusha neema ya kuokoka na kuangamia lau kama si rehema yake na usaidizi wake. Wala hapana wa kuwasaidia, wala hawaokolewi, na kuangamia kadiri watakavyotaka usaidizi.

Isipokuwa kwa rehema zitokazo kwetu na starehe kwa muda.

Yaani isipokuwa Mwenyezi Mungu akiwawahi kwa rehema yake na kuwaakhirisha hadi muda malum kulingana na ujuzi wake na hekima yake.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اتَّقُوا مَا بَيْنَ أَيْدِيكُمْ وَمَا خَلْفَكُمْ لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ {45}

Na wanapoambiwa: Ogopeni yalioko mbele yenu na yaliyoko nyuma yenu, ili mpate kurehemewa.

وَمَا تَأْتِيهِمْ مِنْ آيَةٍ مِنْ آيَاتِ رَبِّهِمْ إِلَّا كَانُوا عَنْهَا مُعْرِضِينَ {46}

Na haiwafikii Ishara yoyote katika Ishara za Mola wao ila wao huwa ni wenye kuipuuza.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ أَنْفِقُوا مِمَّا رَزَقَكُمُ اللَّهُ قَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِلَّذِينَ آمَنُوا أَنُطْعِمُ مَنْ لَوْ يَشَاءُ اللَّهُ أَطْعَمَهُ إِنْ أَنْتُمْ إِلَّا فِي ضَلَالٍ مُبِينٍ {47}

Na wanapoambiwa: Toeni katika aliyowapa Mwenyezi Mungu, waliokufuru huwaambia walioamini: Je! Tumlishe ambaye Mwenyezi Mungu angependa angelimlisha? Nyinyi hammo ila katika upotofu ulio dhahiri.

وَيَقُولُونَ مَتَىٰ هَٰذَا الْوَعْدُ إِنْ كُنْتُمْ صَادِقِينَ {48}

Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi ni wakweli?

مَا يَنْظُرُونَ إِلَّا صَيْحَةً وَاحِدَةً تَأْخُذُهُمْ وَهُمْ يَخِصِّمُونَ {49}

Hawangojei ila ukelele mmoja tu utakaowachukua nao wanazozana.

فَلَا يَسْتَطِيعُونَ تَوْصِيَةً وَلَا إِلَىٰ أَهْلِهِمْ يَرْجِعُونَ {50}

Basi hawataweza kuusia, wala hawatarejea kwa watu wao.

وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَإِذَا هُمْ مِنَ الْأَجْدَاثِ إِلَىٰ رَبِّهِمْ يَنْسِلُونَ {51}

Na itapulizwa Parapanda, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao.

قَالُوا يَا وَيْلَنَا مَنْ بَعَثَنَا مِنْ مَرْقَدِنَا ۜ ۗ هَٰذَا مَا وَعَدَ الرَّحْمَٰنُ وَصَدَقَ الْمُرْسَلُونَ {52}

Watasema: Ole wetu! Nani aliyetufufua malaloni petu? Haya ndiyo aliyoyaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume.

إِنْ كَانَتْ إِلَّا صَيْحَةً وَاحِدَةً فَإِذَا هُمْ جَمِيعٌ لَدَيْنَا مُحْضَرُونَ {53}

Haitakuwa ila ukelele mmoja tu, mara wote watahudhuruishwa mbele yetu.

فَالْيَوْمَ لَا تُظْلَمُ نَفْسٌ شَيْئًا وَلَا تُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كُنْتُمْ تَعْمَلُونَ {54}

Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa ila yale mliyokuwa mkiyatenda.