Dibaji
Mtukufu Mtume (s.a.w.) asema:
"Ee Allah! Hawa (Ali, Fatima, Hasan na Husein) ndio Ahlul-Bayt wangu, basi watoharishe kwa tohara kamili."
"Husein anatokana na mimi na mimi ninatokana na Husein..."
"Hao (Hasan na Husein) ni maua yangu katika dunia."
"Ewe Mwanangu (Husein)! Mwili wako ni mwili wangu na damu yako ni damu yangu.."
"(Ewe Husein), wewe u Sayyid, mwana wa Sayyid, na ndugu wa Sayyid; wewe u uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu) mwana wa uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu) na ndugu wa uthibitisho (wa Mwenyezi Mungu); na baba wa uthibitisho tisa ambao wa tisa wao ni Qaim wao ambaye atakuwa al-Mahdi. "
"Hasan na Husein ni Masayyidi wa Vijana wa Peponi."
"Ewe Mola wangu! Mpende yule ampendaye Husein."
"Adhabu atakayoipewa yule mwuaji wa Husein huko Motoni itakuwa sawa na nusu (nzima) ya adhabu yote watakayoipewa wenye dhambi waulimwengu."
" Allah hujirafikisha na wale wajirafikishao na Husein, yu adui wa wale walio maadui zake."
******
Ahlul-Bayt (a.s.) Assembly ya Tanzania (ABATA) ina furaha kutoa kitabu kama hicho cha Majlis kwa watu wazungumzao Kiswahili. Allamah Sayyid Saeed Akhtar Rizvi, Mwenyekiti wa ABATA, amekichagua kwa ajili ya madhumuni hiyo kitabu kiitwacho "Muqaddamah al-Majalis al-Fakhirah fi Ma'atim al-Itrah at Tahirah" kilichoandikwa na mwanachuoni mashuhuri wa dini na mtunzi, marehemu Allamah Sayyid Abdul Husein Sharafuddin al-Musawi, wa Jabal Amil (Lebanon).
Shaykh Musabah Shaban Mapinda, wa Dar-es-Salaam, kwa ushauri wa Mwenyekiti wa ABATA amefanya tarjuma ya kitabu hiki kutoka Kiarabu kwenda kwenye Kiswahili, kinachoitwa "Maombolezo ya Kifo cha Imam Husein (a.s.)."
Hiki ni kitabu cha pili ambacho kinatolewa na Ahlul-Bayt (a.s.) Assembly ya Tanzania; na tunayo furaha kubwa kwa kutoa kitabu cha Majlis ambacho ni cha kwanza katika lugha ya Kiswahili.
Allah Subhanahu wa Ta'ala atoe malipo yake kwa mtunzi, mfasiri na wale wote ambao wamesaidia katika uchapishaji wake kwa njia yoyote.
Wa ma Tawfeeqi illa Billah.
P.O. Box 75215,
Dar-es-Salaam, Tanzania
24 April, 1998
F.A. Hameer
Katibu Mkuu
Ahlul-Bayt (a.s.) Assembly ya Tanzania